KATEKISIMU YA KANISA KATOLIKI



KATEKISIMU YA KANISA KATOLIKI

UTANGULIZI

KATEKISIMU NI NINI?

Ni muhutasari wa mafundisho yote ya kanisa katoliki mintarafu imani na maadili.

KATEKISIMU INA TABIA GANI ?


Ina tabia ya kuleta na kuonyesha kwa uaminifu kabisa na kwa mpangilio wa hatua kwa hatua mafundisho ya maandiko Matakatifu, Mapokeo ya kanisa,Mafundisho rasmi ya Kanisa na pia urithi wa kiroho wa mababa,walimu na Watakatifu wa kanisa.

KATEKESI NI NINI?

Ni jumla ya jitihada na njia zote za kanisa za kuwaingiza,kuwaunda na kuwakomaza waumini wake, wapya au waliokwisha kuwa tayari waumini,ikiwa ni njia ya kuwasaidia hao wafikie kuamini kweli kuwa YESU KRISTU ni Mwana wa MUNGU, na kwa kuamini hivyo wapate uzima wa milele kwa njia ya huyu YESU KRISTU.

KATEKISTA NI NANI?

Katekista ni mwumini aliyeitwa na Mungu, akateuliwa na Kanisa,kulingana na mahitaji ya kanisa la mahali, ili afanye Kristu ajulikane, asadikiwe, apendwe na afuatwe na wale wasiomjua bado na hata na waumini wenyewe hasa katika hatua za msingi na awali za ufuasi wa Kristu.

MKATEKUMENI NI NANI ?


Kimsingi Mkatekumeni ni yule mtu ambaye hajabatizwa bado, lakini ameleta rasmi ombi lake la hiari la kutaka kubatizwa na hivyo kutaka kujiunga na kanisa, ameanza rasmi kujiandaa kwa ajili ya maisha hayo mapya ya imani kwa kufuata mafundisho ya msingi ya dini, na pia ameanza kujifunza kufuata hatua za kwanza za maisha ya kikristu na maadhimisho ya mafumbo matakatifu; Mtakekumeni wa aina hii ni yule anayejiandaa kwa ubatizo. au kiuchungaji mkatekumeni ni kila mmoja anayejiandaa kwa kufuata mafundisho maalum ili kupokea mara ya kwanza sakramenti yeyote ile inayomwingiza katika ukristu au kumkamilisha katika ukristu.

SEHEMU YA KWANZA - IMANI


KANUNI YA IMANI

Yatupasa kusadiki uwepo wa Mungu Mwenyezi aliye hai na yote yaliyofunuliwa na Mungu.

Mungu amejifunua kwetu kwa namna gani?

Kwa ulimwengu aliouumba

kwa dhamiri ya kila mtu

kwa maandiko matakatifu

kwa mapokeo matakatifu

kwa njia ya Yesu Kristu aliye ufunuo mkamilifu na wa mwisho

Kanisa katoliki huchota mafundisho ya Mungu wapi?

Katika maandiko matakatifu

Katika mapokeo matakatifu

Mungu ni nani?

Mungu ni muumba wa mbingu na dunia, muumba wa watu na wa vitu vyote na Baba mwema.

Kwanini Mungu ametuumba na kutuweka duniani?

Ili tumjue,tumpende,tumtumikie kusudi mwishoni tufike kwake mbinguni.

Tufanye nini ili tuweze kufika mbinguni ?

Tumsadiki Mungu

Tushike amri zake na za kanisa

Tupokee sakramenti na tusali.

ITAENDELEA....!!! BWANA YESU AKUBARIKI SANA

Comments

Popular posts from this blog

Katekisimu ya Kanisa Katoliki